Wednesday, March 22, 2017

Sumaye awakaanga Magufuli na Makonda

WAZIRI Mkuu mstaafu, Frederick Sumaye amesema Rais John Magufuli amesahau kama amechaguliwa na wananchi jambo linalomfanya kufanya maamuzi yake bila kujali hisia zao, anaandika Hamisi Mguta.

Sumaye alitoa kauli hiyo leo alipozungumza na wanahabari katika ofisi za Kanda ya Pwani za Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema) jijini Dar es Salaam,kufuatia kauli za Rais Magufuli alizotoa jana kuwa, haelekezwi kufanya mambo yake kwani alichukua fomu peke yake, hivyo hakuna anakayemuelekeza katika maamuzi yake.

Sumaye ambaye ni Mjumbe wa Kamati ya Utendaji ya Chadema, amesema, anakubaliana na Rais kuwa ana mamlaka ya kupanga watu wake na hakuna mtu anayeweza kumuingilia katika hilo lakini anatakiwa kutii hisia za wananchi wake.

“Nimemsikia Rais akisema kwamba yeye haambiwi, yeye ndio Rais, ni kweli, akasema alichukua fomu ya kugombea urais yeye peke yake kwa hiyo anatenda kazi zake anavyotaka, ni kweli lakini ni nani alimpigia kura? Ni watanzania ndiyo waliomfikisha pale,” amesema Sumaye.

Amesema, haki itendeke kwenye jambo la Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam, Paul Makonda kuhusishwa na tuhuma mbalimbali na kuwa limezungumziwa na rais, mawaziri na inaonekana mikanganyo ya dhahili na inaonekana pia kuna mtu anabebwa.

“Kama mkuu wa mkoa anafikia mahali anavamia kituo cha habari, waziri anayehusika na habari anakwenda anasikitika, lazima kuna tatizo, mimi Makonda nikisikia hata kesho ameingia mahali amepiga watu makofi wala sitashangaa, ametukana watumishi mbele ya kadamnasi sishangai, kwa sababu kama kweli yale yaliyoandikwa ni kweli, amefika mwisho wa uwezo wake,” amesema.

Makonda amekuwa katika kipindi kigumu cha kukabiliwa na tuhuma nzito za kumiliki vyeti vinavyotajwa kuwa vimetokana na jina la mtu mwingine aitwae Paul Christian, aliyefaulu mtihani wa taifa wa kidato cha nne, Shule ya Sekondari ya Pamba, jijini Mwanza.

Isitoshe, Ijumaa ya wiki iliyopita, alijiongezea mzigo wa kashfa alipofuatana na polisi wenye silahausiku na kuvamia kituo cha habari cha Clouds Media, kilichopo Mikocheni, na kutaka kulazimisha kurushwa kipindi cha Shilawadu kwa namna atakavyo.


No comments:

Post a Comment