Thursday, November 10, 2016

TAARIFA KWA UMMA –UCHAGUZI MKUU WA MAREKANI

TAARIFA KWA UMMA –UCHAGUZI MKUU WA MAREKANI

• Pongezi kwa Rais Mteule
• Ni ushindi wetu IDU

Chama cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA) kinawapongeza wananchi wa Marekani kwa kufanya uchaguzi wao kwa njia ya amani hapo tarehe 09.11.2016, na kukamilisha kampeni za kumpata kiongozi wa Nchi hiyo.

Tunapenda kumpongeza Rais Mteule Mhe. Donald Trump na Chama chake cha Republican ambao ni wanachama wa IDU kwa ushindi wa kihistoria walioupata, na zaidi tunampongeza rais mteule Trump kwa hotuba yake ya awali ya kuwashukuru wananchi wa Marekani na hasa aliposema kuwa anaahidi kwa wananchi wote wa Marekani kuwa anaenda kuwa rais wa wote, na kuwa hilo ni jambo la umuhimu wa kipekee kwake.

“I pledge to every citizen of our land that I will be President for all Americans and this is so Important to me”.

Ushindi huu ni ushindi wetu sisi wanachama wa Jumuiya ya Kimataifa ya Kidemokrasia (International Democratic Union-IDU)na unatuma salaam nzito kwa Madikteta popote pale walipo kuwa utawala mpya wa Marekani hautavumilia kuona Madikteta ambao wanaminya Demokrasia na Haki za Binadamu, kama alivyoahidi wakati wa Kampeni zake.

Tunaahidi kumpa ushirikiano wote kwenye vikao vya IDU ambavyo sisi tunashiriki kama wanachama wa umoja huu na tutampatia kila aina ya taarifa sahihi kadiri ya uwezo wetu kuhusu hali ya Haki za Binadamu na Demokrasia nchini Tanzania na Barani Afrika.

Mwisho, tunampongeza Hillary Clinton kwa kufanya kampeni za kihistoria na kukubali matokeo ya kura .
Imetolewa leo tarehe 09.11.2016
na;

John Mrema –Mkurugenzi wa Itikadi, Mawasiliano na Mambo ya Nje.

No comments:

Post a Comment