Friday, September 9, 2016

MHESHIMIWA RAIS AJIONDOE KWENYE HILI LA KUHUJUMU MAMEYA WA UPINZANI.

Ndugu wananchi na wakazi wa *Manispaa ya Kinondoni*, nianze kumshukuru Mwenyezi Mungu kwa kutuepushia mabalaa na kutujalia Afya njema.Hatuna la kumlipa zaidi ya kusema ahsante.



Leo nimeamua kuita vyombo vya habari ili kuhabarisha uma na watanzania wote kwa dhumuni moja tu, la kuelezea masikitiko yangu dhidi ya Utawala huu wa awamu ya tano, ambapo mimi Mstahiki Meya wa kinondoni, nalazimika kwa namna moja kufanya nao kazi ya kuhudumia wananchi.

Naleta masikitiko yangu kwenu si kwa lengo la kuchochea hasira za watu bali kuonyesha, gilba, uzandiki, fitina na uchonganishi tunaokutana nao kutoka kwa viongozi wa serikali ya Awamu ya tano.

Ndugu wananchi lazma tuweke rekodi wazi ya kuwa mimi siyo mteuliwa bali mchaguliwa kutoka kwenye kundi kubwa la viongozi mliowachagua October 2015, hivyo mabosi wangu ni nyinyi na pakushtaki ni kwenu yani uma, ili mnitendee sawa na mapenzi yenu mliyonituma kuwaletea maendeo.

1.KWA MASIKITIKO SERIKALI YA JAMHURI YA MUUNGANO WA TANZANIA, IMEANDIKA BARUA KUKATAA MANISPAA YA KINONDONI TUSIPEWE MSAADA WA MRADI KIWANDA CHA KUCHAKATA TAKATAKA ZIWE MBOLEA, KUTOKA SERIKALI YA UJERUMANI, UNAOGHARIMU KIASI CHA SHILLINGI BILLIONI 3.2.

Kosa letu kubwa ni msaada kutoka wakati huu ambapo manispaa ya kinondoni ina shikiliwa na wapinzani(UKAWA) na kuonekana kwamba mradi huu ungetujenga binafsi na siyo CCM, kukataa huku ni kwa kuandikia barua wahisani hao kwamba mitambo na vitu vyote wanavyo panga kutuletea, vitozwe kodi, ambayo itagharimu kiasi cha sh millioni 900.

Ikumbukwe mradi huu ni msaada tu na siyo biashara na kwamba baada ya assembly ya mitambo, wajerumani walikuwa wanaikabidhi manispaa ya kinondoni ndani ya miezi 6, kitendo hiki siyo tu kutukwaza sisi kama wapinzani, ila kimewakwaza wahisani. Wahisani hao kutoka ujerumani wamejitolea kutusaidia billioni 3.2, ukiongeza millioni 900, tafsiri yake tunawalazimisha watusaidie billioni 4.1, huo si uungwana hata kidogo.

Nani asiyejua mchakato wa mradi huu ulianza sikunyingi kabla ya wapinzani kuongoza manispaa ya kinondoni, ila mradi umekuwa hai kipindi cha wa pinzani kwa sababu ya sifa yetu kubwa ya kutokuwa warasimu.

Ndugu wananchi hili limetusikitisha sana hasa kwa serikali hii inayo jipambanua ya kutetea wanyonge na HAPA KAZI TU.

Kushindwa kujua kuwa mradi huu ulikuwa unakuja kufanya mapinduzi makubwa ya hali ya USAFI si kinondoni tu bali DAR ES SALAAM yote kama jiji..

Jiji letu lingekuwa safi na wananchi wangeondokana na michango ya takataka,sababu mradi huu ulikuwa umelenga kutoa magari ya taka kupita mtaani nakuzikusanya bure.

2.JUU YA UJIO WA MHESHIMIWA RAIS NDANI YA MANISPAA YA KINONDONI.

Nimeona nilitolee ufafanuzi hili suala baada ya kuona napigiwa sana na kutumiwa ujumbe kwa njia ya simu, watu wakitaka kujua ukweli wa mambo juu ya lililotokea siku ya 06-09-2016.

Siku hiyo niliomba Madiwani waliokuwa wana kikao cha kamati ya mipango miji kuja kujumuika nasi ingawa itifaki na mpangilio wa tukio ulikuwa kichama zaidi (Ki-ccm) kuliko kiserikali. Mimi mweneyeji kwenye manispaa yangu wakanikalisha nyuma siti ya tatu kutoka meza kuu, huku viongozi wa CCM kama Mwenyekiti wa Mkoa na wengine wakikaa mbele yangu.

Zaidi ni kwamba ujio huo wa Mheshimiwa Rais sikuwa nimetaarifiwa na taasisi yoyote ya Serikali, kuanzia Ikulu, Mkoa mpaka wilaya, isipokuwa niliona busara kwakuwa maandalizi yaliyoendelea yalifanyikia getini kwangu, si vyema kama muungwana kuacha kwenda kujumuika na Mheshimiwa Rais, isingeleta picha nzuri kwa kiongozi kama mimi.

Pili, kukosekana kwangu kwenye ratiba kusalimia au kuongea na Wananchi wangu wa Kinondoni pia nako kulinifanya nishangae zaidi; iweje mwenyeji nisiwepo kwenye ratiba hiyo huku watu mbalimbali wakipata fursa ya kuzungumza ama kusalimia watu wa kinondoni.

Tatu, kupangwa kwa mtu maalumu wa kunitukana mimi mbele ya Rais ambaye amekiri kuwa alikutana na mkuu wa mkoa kwanza na kukubaliana kuwa ataongea huku tayari risala kwa niaba ya wahusika ikiwa imeshatolewa.

Nne, upotoshaji mkubwa uliofanywa na waziri Lukuvi; kwamba manispaa ionekane tulitesa wakazi hao na kuwatapeli bila ya msaada wowote, mpaka wao walipo amua kuja kuongea nao.

YOTE HAYA yalionyesha ni
namna gani viongozi hawa walijipanga kumpotosha Mheshimiwa Rais na kutosema kweli kwa dhumuni la kulaghai ama kuchafua taswira ya Manispaaa ya kinondoni kwakuwa inaongozwa na wapinzani.

Kimsingi Waziri Lukuvi na Mkuu wa Mkoa walikuwa na kila sababu ya kuzuia nisipate japo dakika moja kusema ukweli juu ya mradi ule wa nyumba kongwe magomeni kota. Mradi ule ni sawa na miradi ya wilaya zingine Dar es salaam ambapo Temeke waliokuwa wapangaji waliondoka kwa hiari bila kulipwa chochote wakati Ilala mpaka sasa wapangaji na manispaa wapo mahakamani. Kinondoni pekee ndiyo ilikuwa imewalipa wapangaji wake pesa ya kodi ili kupisha ubomoaji.

Wakati huo wapangaji hao walikaa kwa muda wa miaka 10 bila ya umeme wala maji, baada ya Mahakama kuamuru kuwa yalikuwa ni makazi hatarishi.

Lakini Mheshimiwa Rais si kweli kwamba ardhi ile ilipangwa kuuzwa isipokuwa Mheshimiwa Rais Mstaafu Jakaya Mrisho kikwete alichukua baadhi ya madiwani na kuwapeleka Indonesia ziara ya kiserikali na baadaye wakaenda Romania, huko ndiko walipokuja na mwekezaji anayeitwa Blue Marine kutoka Romania, ambao walikubali kuwajengea wakazi hao 644 nyumba na kuwarudisha kama wapangaji huku wakitengeneza majengo mengine ya biashara, makao makuu mapya ya Halmashauri ya Manispaa ya Kinondoni, kuvunja Shule ya msingi pembeni ya magomeni kota ili kuijenga upya; Blue Marine walikwama kungoja saini ya waiziri wa Tamisemi tangu 2014.

Na kama Rais leo akiitisha documents hizo kutoka Tamisemi ataona mapendekeo ya mkataba kati ya manispaa ya kinondoni na BLUE MARINE. Kusema ardhi ilikuwa imeuzwa ni upotoshwaji mkubwa uliofanywa na waziri Lukuvi huku akijua kuwa yeye akiwa Waziri awamu ya nne,chini ya Rais Kikwete tayari uwekezaji wa magomeni kota likua umesha anza, isipokuwa sheria inatutaka tumpe Waziri ili aweze kuidhinisha.

Waziri Lukuvi kusema kuwa mradi huu ulikuwa ni wa utapeli hatukomoi UKAWA bali tuna mshangaa kwa kumzushia shutuma hizo Rais kikwete, na akitaka kujua ukweli wa mradi hata pale Rais alipo mtuma aje afuatilie swala hilo.

Mheshimiwa Rais nilitaka nipate fursa nikueleze kuwa Mawaziri wote wa Ardhi walisha wahi kutaka kupora eneo hilo. Badala ya kukutana na Halmashauri akaona ni vema apate fursa ya kuitisha hati za Halmashauri na kuzifutilia mbali.

Mheshimiwa Rais kila mtu anaunga mkono juhudi za kuwasaidia wazee au wakazi wale wa nyumba kongwe ila kupotosha umma na kuliko fanywa na Waziri kulikuwa na lengo binafsi la kutaka kunufaika na mradi mpya utakao anzishwa.

Hasara kubwa iliyopatikana baada ya kufutwa hati za eneo hilo ni kwamba serikali za mitaa zimeondolewa maeneo ya uwekezaji ambayo yangesaidia kuimarisha makusanyo ya Halmashauri na kufanya serikali hizi za mitaa ziwe tegemezi baada ya kuporwa vyanzo vyake vya mapato. Baaada ya mwekezaji kujenga na kuwapatia makazi wapangaji wale palikuwa na kituo kikubwa cha uwekezaji kianzishwe.

Lakini si hilo tu; tayari benki ya dunia walikuwa wametoa fedha za kumpatia mkandarasi mshauri(consultant) GUff GMB kutoka ujerumani kiasi cha dola laki nne na themanini kutuandalia michoro ya jengo la utawala kwa ajili kuiwezesha Manispaa miongoni mwa majengo yaliyokuwa yanategemewa kutoka kwenye mradi wa viwanja hivyo vilivyo chukuliwa.

Mheshimiwa Rais nimalizie kuwa, ningepata walau dakika tatu ningekueleza jinsi Waziri wako Lukuvi alivyo hatari san, na Manispaa ya Kinondoni mpaka leo inaonja machungu yake aliyotusababishia kukosa kiasi cha shillingi zaidi billioni ya 12, ningekufafanulia na kukuomba utumie vyanzo vyako vya usalama kudhibitisha.

Nishukuru kuwa hata walichopanga pia kukifanikisha uliruka kiunzi baada ya kusema wakujenga bado haujaamua, tofauti ya Waziri Lukuvi kujiandaa na watu wake kupokea eneo hilo, imani yangu hata kama tumeporwa bado lipo salama sana, kuliko ungemkabidhi yeye ndiye achukue ardhi hiyo ili ekari mbili ajenge flats za hao 644, zingine wajanja wa mjini watumie kwa mambo yao.

Mwisho nataka kumwambia Mheshimiwa Rais ya kuwa Wabunge, Madiwani na Mameya tunakuja kwenye ziara zako tukijua ni ujio wa kiserikali, lakini kama kiongozi Mkuu wa nchi tunataka uwaonye viongozi wako waache kufanya ziara zako kuwa za kichama kuliko serikali.

Mheshimiwa Rais usishangae Ikafika muda usituone katika ziara zako zingine kama baadhi ya viongozi wa serikali kutaka kuchanganya uccm na ziara ya kiserikali; au kuona mtu kama mkuu wa Mkoa akiongea vijembe kuwa eti ni "mbabe wa vita"..ubabe dhidi ya nani? Na ni vita ipi? matusi yale mbele yako tafsiri itakuja kuwa unawatuma au kuwapanga mapema kutoa matusi na mipasho, sisi mameya tutaendelea kuwa ni waungwana.

Sisi Mameya wa upinzani tumefikia mwisho, Wabunge na Madiwani kwenye ziara zako, tukiona hatutambuliwi kama Viongozi wa Wananchi tuliochaguliwa,na wanachi badala yake nikuona fedheha za kuita makada wa ccm watutukane.

Yaani tulienda mbele za wananchi na kuwaomba kura kwa unyenye kevu, kama akitaka kuonyesha ubabe basi aje agombee kata ya ubungo.




No comments:

Post a Comment