Wednesday, September 21, 2016

DIWANI WA CHADEMA TEMEKE AFUKUZWA UANACHAMA KWA TUHUMA ZA RUSHWA

September 19, 2016 Chama cha Demokrasia na Maendeleo CHADEMA jimbo la Temeke kimemfukuza uanachama Diwani na Mwenyekiti wake kutoka kata ya Kurasini, Matiti Claudian Togocho kutokana na kashfa ya ufisadi wa zaidi ya shilingi milioni 400 alizozipata kwa njia ya udanganyifu.

Taarifa iliyotolewa na Benard Mwakyembe ambaye ni Mwenyekiti wa Chadema wilaya ya Temeke imeeleza kuwa mnamo November 23 2015, Diwani huyo akiwa na wenzake wanadaiwa walitengeneza hati feki ya nyumba tano za James Makundi aliyekuwa mpangaji kwenye nyumba zake kisha kufanya hujuma ya kuvunja nyumba hizo kwa amri ya uongo ilitolewa na wakili kishoka wa Samora Avenue badala ya amri ya mahakama ikiwa ni kwa lengo la kujipatia pesa kutoka kwa mwekezaji ambazo ni zaidi ya shilingi milioni 200.

Diwani huyu pia anahusishwa na matukio mengine mawili ya udhulumaji wa zaidi ya shilingi milioni 140 za mirathi ya marehemu Peter Christian Kijeni wakati kesi ikiwa mahakamani pamoja na fedha za fidia za Paulina Shaban na wajukuu zake ambao Diwani huyo alisimamia nyumba zao kubomolewa.

"Kutokana na maamuzi ya chama baada ya kujiridhisha na makosa yake na kwa mujibu wa katiba ya chama chetu, mamlaka za mwisho zimefikia maamuzi ya kumvua uanachama wake hivyo atakuwa amepoteza sifa za kuwa Mwenyekiti wa Serikali ya mtaa wa Mivinjeni pamoja na nafasi yake ya Udiwani kata ya Kurasini." Alisema Benard Mwakyembe

No comments:

Post a Comment