Saturday, December 6, 2014

Mbowe: Tutazuia uchaguzi wa Mitaa mahakamani ikiwa...

Dar es Salaam.
Mwenyekiti wa Chadema, Freeman Mbowe amesema kama hali ya kuwaengua wagombea wa chama hicho katika uchaguzi wa Serikali za Mitaa itaendelea kama ilivyo sasa, basi wataupinga uchaguzi huo mahakamani.
Mbowe alisema hayo jana katika mkutano wa hadhara wa operesheni mshikemshike mzizima uliofanyika Vijibweni Kigamboni.
“Tangu kampeni zianze kumekuwa na tabia ya kuengua wagombea wetu kiholela. Tumeshaweka angalizo mahakamani na kama hali ikiendelea hivyo tutaupinga uchaguzi mahakamani.”
Alisema baada ya kuibuka kwa tabia ya wagombea kuenguliwa aliwasiliana na Waziri Mkuu, Mizengo Pinda akimsihi alitizame kwa kina suala hilo kwa sababu wagombea walienguliwa kimakosa.
“Alisema atalifanyia kazi lakini naona bado hali hiyo inaendelea na alisema atazungumza na Katibu Mkuu wa CCM, Abdulrahman Kinana kuhusu jambo hili.
Nilipowasiliana naye mara ya pili alisema kama tunataka ushindi uchaguzi uwe wa haki. Kuona hivyo tumekwenda kutoa angalizo mahakamani,” alisema.
Aliongeza, “Tukutane katika uchaguzi na tuone nani ni bingwa kati ya CCM na Ukawa baada ya kutumia njia za mkato kama wao wanavyofanya.
Hata sisi hatutaki ushindi wa dezo ila wakitumia dola kutuyumbisha kamwe hatutokubali maana polisi wamekuwa wakitumika kama mawakala wa uchaguzi. Hilo halitakubalika.”
Aliwataka wananchi kutokaa mbali na vituo vya kupigia kura mara baada ya kuwachagua viongozi wanaowataka huku akisisitiza, “Msikubali kura zikahesabiwe sehemu nyingine watazichakachua.
Hata katika sheria za Uchaguzi hakuna sehemu inayosema baada ya kupiga kura, mpigakura anatakiwa kukaa umbali wa mita 100 kutoka katika kituo cha kupiga kura. Tumeweka mawakala nchi nzima kuhakikisha kila kitu kinakuwa sawa.”
Alisema hakuna dhambi mbaya kama wananchi kushindwa kuleta mapinduzi ndani ya nchi yao, hasa nchi kama Tanzania ambayo ina kila aina ya umasikini.

1 comment:

  1. wapiga kura angarieni wagombea wengine katika uchaguzi wa serikari za mitaa hasa Ostabei si wakazi harisi bari mapandikizi......angaria vizuri mtaa wa bangoyo

    ReplyDelete