Sunday, December 14, 2014

Lema avamiwa na ‘UVCCM’, gari yake yasuliwa vioo; alazimika kufyatua risasi tatu hewani kujiokoa!

Gari la Godbless Lema lililovunjwa kioo huko Clock Tower, Arusha

Mbunge wa Arusha Mjini Mh Godbless Lema amekubwa na tukio la aina yake maeneo ya Clock Tower Jijini hapa ambapo vijana wanaoaminika kuwa vijana “wafuasi wa UVCCM” walishamshambulia kwa mawe na kufanikiwa kuvunja kioo cha nyuma ubavuni cha gari la Mbunge huyo.

Tukio hilo la kustaajabisha na kutiasha katika swala la amani na usalama kipindi hiki cha kampeni za Serikali za mitaa lilitokea kwenye Sheli iliyopo mkabala na New Arusha Hotel majira ya jioni saa moja ambapoMbunge Lema akiwa na dereva wake na mtu mwingine mmoja walijikuta wakishambuliwa vikali na watu ambao Mh Lema amethibitisha ni vijana waliokuwa kwenye msafara kampeni.

Blog hii ilifanikiwa kufika Kituo Kikuu cha Polisi Jijini Arusha usiku wa saa tatu na kumkuta Lema na wafuasi wa Chadema zaidi ya 200 wakiwa na viongozi wao katika kituo hicho kikuu kwa ajili ya kutoa maelezo na taratibu nyingine za kipolisi zifuate.

Akisimulina namna ilivyokuwa, Lema alisema kuwa muda huo akiwa garini kuelekea nyumbani alimuona kijana mmoja anapigwa sana na vijana hao wa CCM wakiwa na sare za chama. Anasema kijana huyo alikuwa anapigwa mno na kuburuzwa kupelekwa maeneo ya mtoni ambapo alihisi angeweza kuuawa.

Lema akamuamuru dereva wake kusimaiisha gari na mtu mwingine waliyekuwa nae kwenye gari akashuka kumuokoa kijana yule. Baada ya kufanikiwa kuwatenganisha na kuwashikilia vijana wawili wa CCM waliokuwa wanampiga yule kijana, kundi kubwa la vijana wengine wakiwa na silaha na mawe walishuka kutoka kwenye Lori walilokuwa wakisafiria kutoka kwenye kampeni na kumvamia wakijaribu kuwaokoa wenzao kuondoa ushshidi. Lema akalazimika kupiga risasi ya kwanza hewani wakarudi nyuma kama hatua kadhaa.

Baada ya sekunde kadhaa wakarudi tena kumzonga Lema huku wakirusha mawe na silaha nyingine. Mawe yale yalijaeruhi baadhi ya watu waliokuwa jirani pamoja na mhudumu wa Sheli hiyo kupigwa marungu na Lema hakujua hali yake ikoje.

Walivyozidi kumshambulia na mawe na silaha nyingine na kufanikiwa kuvunja kioo cha gari yake, Lema alifyatua tena risasi ya pili na ya tatu kuwatawanya na akawasiliana na Polisi ambapo kituo hakiko mbali lakini anasema simu ya OCD na OCS hazikuweza kufanya mawasiliano.

Akalazimika kuwafuata askari Kituo Kikuu na kwa pamoja wakarudi eneo la tukio na kuwakuta vijana wale bado wako wanaimba nyimbo za kusifu chama chao.

Lema anasimulia kuwa vijana wale walimdhihaki OCD wakimuimbia nyimbo kwa shangwe ambaye pamoja na askari wake hawakuweza kumkamata hata mtu mmoja wala kukamata gari hilo.

Baadae ndio akarudi kituoni kutoa maelezo huku wafuasi wa Chadema wakishinikiza kama Polisi hawawezi kuwakamata watu hao usiku huo basi wawaachie kazi hiyo waifanye wao wenyewe kuhakikisha kabla hakujakucha watu wote wametiwa nguvuni kwasababu wanajulikana!

Mpaka Blog hii inaondoka kituoni hakukuwa na kukamatwa kwa mtu yeyeote zaidi ya askari Polisi na viongozi wa Chadema kusaidiana kutafuta maganda ya risasi eneo la tukio.

Polisi bado hawajatoa taarifa yeyote kuthibitisha tukio hilo!

No comments:

Post a Comment